Msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Russia, Igor Konashenkov amesema kuwa, shambulio lolote la kombora au la anga litakalolenga maeneo ya jeshi la serikali ya Syria, litakuwa linahatarisha majeshi ya Russia na Syria kwa pamoja.
Konashenkov ameitaka Marekani kuzingatia kwa umakini matokeo mabaya yatakayotokana na hatua yake ya kushambulia maeneo ya jeshi la Syria.
Ameingeza kuwa, baada ya hujuma ya anga iliyofanywa na ndege za kivita za Marekani tarehe 17 Septemba dhidi ya jeshi la Syria, Moscow ilichukua hatua za lazima za kuzuia kujikariri tukio kama hilo dhidi ya jeshi lake nchini Syria.
Msemaji wa Wizara ya Ulinzi nchini Russia, amesisitiza kuwa, ni wakati kwa Marekani kufahamu kwamba, ngao ya anga ya Russia haitakuwa na wakati wa kuangalia sehemu ilipotokea hujuma, bali itajibu haraka shambulio lolote lile. Igor Konashenkov amebainisha kwamba, sehemu ambazo zinaweza kulindwa na ngao za kujilinda kwa makombora za S300 na S400 nchini Syria ni pamoja na kambi mbili za kijeshi za Hamim na Tartus.
No comments:
Post a Comment