Friday, October 7

WAFANYABIASHARA WA DRC WAIPONGEZA SERIKALI YA TANZANIA.

k1
Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Congo (DRC) nchini Tanzania Bw. Sumail Edward (kulia) akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari kuhusu uamuzi wa wafanyabiashara wa Congo kutumia Bandari ya Dar es Salaam baada ya Serikali kuondoa vikwazo, kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari  Bw. Tiganya Vincent.
k2
Baadhi ya waandishi wa habari wakimfuatilia kwa makini Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Congo (DRC) nchini Tanzania Bw. Sumail Edward (mwenye suti) wakati alipokuwa akielezea kuridhika na uamuzi wa Serikali ya Tanzania kuondoa vikwazo katika Bandari ya Dar es Salaam na kupelekea wafanyabiashara wa Congo (DRC) kuendelea kuitumia bandari hiyo.

Picha na Eliphace Marwa – Maelezo
Na: Frank Shija, MAELEZO.
WAFANYABIASHARA kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wafurahishwa na hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kuondoa vikwazo vya usafirishaji wa mizigo kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Hayo yamebainishwa na Rais wa Wafanyabiashara wa Congo waishio nchini Tanzania Bw. Sumaili K. Edward alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kurejea kwao na kutumia Bandari hiyo leo Jijini Dar es Salaam.
Sumaili amesema kuwa miaka ya nyuma kulikuwa na changamoto nyingi ambapo alizitaja kuwa ni mizani na sehemu za ukaguzi kuwa nyingi pamoja na siku za kuhifadhi mizigo kuwa chache.
Alisema kuwa wamefikia uamuzi wa kuendelea kutumia Bandari ya Dar es Salaam baada ya Serikali ya Awamu ya Tano kutatua changamo hizo ambapo sasa vizuizi vimepungua.
“Naipongeza Serikali ya Tanzania kwa hatua ya kutuondolea usumbufu sisi wafanyabiashara wa Congo tuliokuwa tunafanya shughuli zao Bandari ya Dar es Salaam, tumerejea na tutapitishia mizigo yetu hapa”. Alisema Sumaili.
Adhai alisema kuwa wamefarijika kuona sasa siku za kuhifadhi mizigo kabla ya kuongezeka kutoka  siku 15 zilizokuwepo awali hadi kufikia 30 kama ilivyobainishwa wakati wa ziara ya siku tatu ya Rais wa Jamhuri wa Kidemokrasia ya Congo Joseph Kabila mapema wiki hii.
Akijibu swali la la mwandishi wa habari aliyetaka kujua sababu zilizowafanya kusitisha kwa muda kutumia Bandari ya Dar es Salaam, Rais huyo alisema kuwa kitu kikubwa kilicho wafanya wachukue uamuzi wa kusitisha ni gharama kuwa kubwa hivyo kupelekea kufanya biashara isiyokuwa na faida.

No comments: