Sunday, January 31

Wawindaji haramu wamuua rubani nchini Tz


Shirika moja la wakfu wa utunzaji wa mazingira, linasema kuwa rubani mmoja raia wa Uingereza, amepigwa risasi na kuuawa nchini Tanzania.
Rubani huyo anasemekana kuwa alikuwa akipepeleza mzoga wa ndovu porini alipodunguliwa na mwindaji haramu aliyekuwa amejificha .
Operesheni hiyo ilikuwa katika mbuga ya wanyama pori ya Maswa Kaskazini mwa Tanzania.
Shirika hilo lenye makao yake nchini Marekani- The Friedkin Conservation Fund, linasema kuwa rubani Roger Gower, alikuwa akiwasaidia utawala nchini Tanzania kukabiliana na wawindaji haramu katika maeneo ya Serengeti, aliposhambulia .
Maafisa wakuu wa serikali ya Tanzania, wanasema kwamba bwana Gower alifaulu kutua helikopta hiyo lakini akafariki muda mfupi baadaye kutokana na majeraha ya risasi.


Hadi sasa hakuna aliyekamatwa kwa mauaji hayo.
Inaaminika kuwa mvamizi alikuwa na bunduki yenye uwezo mkubwa kwani iliweza kupenya ubavu wa ndege hiyo na kumjeruhi marehemu.
Familia ya marehemu inatarajiwa nchini Tanzania hii leo kuandaa mipango ya maziko.
Hivi karibuni, utawala nchini Tanzania umekuwa ukikosolewa kwa kushindwa kutoa maelezo ya kina kuhusiana na uwindaji haramu wa pembe za ndovu.
Uwindaji haramu umeenea sana katika pori ya Maswa na sio tukio la kwanza ambapo wanaharakati wanaolinda wanyama wa porini wanashambuliwa na wawindaji haramu.
bbcswahili.com

No comments: